Nav bar

Alhamisi, 7 Machi 2024

TALIRI WEST KILIMANJARO KUWA KITIVO CHA UBORA UZALISHAJI MBUZI, KONDOO.


Ni kufuatia matokeo mazuri ya utekelezaji wa mradi wa ECF

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Daniel Mushi amesema kuwa Wizara yake inakusudia kukifanya kituo cha Utafiti wa Mifugo kanda ya Kaskazini cha West Kilimanjaro kuwa kitivo cha Ubora kwenye uzalishaji wa mbuzi na kondoo walioboreshwa kwa ajili ya kuwapa wafugaji nchini ili waweze kufuga kwa tija.

Prof. Mushi amesema hayo leo Machi 05, 2024 baada ya kufika kwenye kituo hicho kilichopo chini ya Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) ambapo ameweka wazi nia ya Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuongeza kiwango cha nyama bora inayouzwa nje kupitia kituo hicho.

"Kama mnavyotambua nchi yetu kwa sasa imeongeza kasi katika kusafirisha nyama nje ya nchi na zaidi ya asilimia 90 ya nyama tunayopeleka huko ni ya mbuzi na kondoo hivyo tuna kila sababu ya kuongeza uzalishaji wa wanyama hao" Ameongeza Prof. Mushi.

Aidha Prof. Mushi amemuelekeza Mkurugenzi wa kituo hicho Dkt. Leonard Marwa na timu yake ya wataalam kuongeza jitihada kwenye utafiti wa mbari, magonjwa, lishe na utunzaji wa mifugo kwa ujumla ili kukifanya kituo hicho kuwa kitovu cha uzalishaji wa mbuzi na kondoo bora watakaokidhi soko la ndani na nje ya nchi.

"Sisi kama Wizara tunaona huu ndo wakati muafaka wa kuifanya nchi yetu kuwa kinara kwenye uzalishaji wa mbuzi na kondoo wengi na sio kwa idadi tu bali kwa ubora pia kwa sababu wataalam tunao, ardhi nzuri tunayo na hali nzuri ya hewa tunayo" Amesisitiza Prof. Mushi.

 Prof. Mushi amesema kuwa kituo hicho pia kitatumiwa na vijana wanaoshiriki programu ya "Jenga kesho iliyo bora kwa wajasiriamali wanawake na vijana upande wa sekta ya mifugo" (BBT-LIFE) ambapo watapata sehemu ya kununua mbari za mbuzi na kondoo bora na ujuzi wa namna ya kuzalisha wanyama hao.

Hatua hiyo ya Serikali kukifanya kituo hicho kuwa kitivo cha ubora kwenye uzalishaji wa mbuzi na kondoo nchini inatokana na mafanikio yaliyopatikana kwenye utekelezaji wa mradi wa ECF ambapo Serikali ilipeleka jumla ya mbuzi na kondoo 465 ili kuzalisha mbegu itakayosambazwa kwa wafugaji nchini.


Mkurugenzi wa Kituo cha Utafiti wa Mifugo kanda ya kaskazini cha West Kilimanjaro Dkt. Leonard Marwa (kushoto) akimueleza Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Daniel Mushi kuhusu utekelezaji wa mradi wa ECF muda mfupi baada ya Prof. Mushi kufika kituoni hapo leo Machi 05, 2024 mkoani Kilimanjaro.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Daniel Mushi akimuangalia mmoja wa ndama wa mbuzi waliozalishwa kupitia mradi wa ECF kwenye kituo cha Utafiti wa Mifugo kanda ya Kaskazini cha West Kilimanjaro muda mfupi baada ya kufika kituoni hapo leo Machi 05, 2024 mkoani Kilimanjaro.


 

SERIKALI YATOA EKARI 1000 ZA RANCHI KWA WANANCHI MKOANI KILIMANJARO

  •  Pia Yawarasimishia ekari 200 walizokuwa wakimiliki awali kinyume na utaratibu.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imewapa wananchi wa kijiji cha Kalimaji eneo lenye ukubwa wa ekari 1000 zilizokuwa zinamilikiwa na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kituo cha West Kilimanjaro kilichopo kanda ya Kaskazini mkoani Kilimanjaro.

Akikabidhi eneo hilo kwa kamati ya Usalama ya Mkoa huo leo Machi, 05, 2024 Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Daniel Mushi amesema kuwa Wizara yake imeridhia kutoa eneo hilo na kurasimisha ekari 200 za awali zilizokuwa zikitwaliwa na wananchi hao kinyume na utaratibu na kufanya kijiji hicho kuwa na eneo lenye ukubwa wa ekari 1200.

"Mhe. Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama sisi kama Wizara tumeridhia kutoa eneo hilo la sehemu ya kituo chetu cha Utafiti cha West Kilimanjaro na tunabariki taratibu zote za kuwamilikisha wananchi wa kijiji hicho ziendelee" Amesisitiza Prof. Mushi.

Akizungumza kufuatia uamuzi huo Mwenyekiti wa kamati hiyo ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe. Nurdin Babu ameipongeza Wizara kwa uamuzi huo ambapo ameongeza kuwa hatua hiyo inaakisi nia ya dhati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan inayolenga kuboresha maisha ya Watanzania kupitia shughuli za uzalishaji kiuchumi zitakazofanywa na wananchi hao kwenye eneo walilopewa.

Uamuzi huo wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kupitia Taasisi yake ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) ni utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa kwenye kikao cha Baraza la Mawaziri kilichoketi Agosti 07, 2021 ambapo kiliamua baadhi ya maeneo ya Serikali kumegwa kwa manufaa ya wananchi ili waweze kuyatumia kwa shughuli zao za kijamii na kiuchumi.



Katibu Tawala wa mkoa wa Kilimanjaro Bw. Tixon Nzunda (katikati) akifafanua jambo kwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Daniel Mushi (wa pili kushoto) na timu ya wataalam kutoka Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) muda mfupi kabla ya makabidhiano ya ekari 1000 za eneo la Kituo cha Utafiti wa Mifugo cha west Kilimanjaro kwa wananchi wa mkoa huo leo Machi 05, 2024.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Daniel Mushi (wa pili kushoto) akifafanua jambo ofisini kwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro Bw. Tixon Nzunda (katikati) muda mfupi kabla ya kuikabidhi kamati ya Usalama ya Mkoa huo ekari 1000 za eneo la  Kituo cha Utafiti wa Mifugo cha West Kilimanjaro  leo Machi 05, 2024.


 

SERIKALI KURASIMISHA BIASHARA YA MABONDO

Na. Edward Kondela

Serikali imesema itahakikisha inachukua hatua ya kuwepo kwa taratibu maalum zilizo wazi kwenye biashara ya mabondo ya samaki ili kujiridhisha upatikanaji wake hadi kufika viwandani kwa ajili ya kuchakatwa.

Akizungumza (05.03.2024) jijini Mwanza na wamiliki wa viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi katika jiji hilo, wakati akimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe, Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh amesema serikali itahakikisha inaweka utaratibu ili kujiridhisha namna ya upatikanaji wa mabondo.

Prof. Sheikh amebainisha hayo baada ya baadhi ya wamiliki wa viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi kulalamika kuwa baadhi ya wavuvi wamekuwa wakivua samaki ambao wako chini ya viwango vinavyotakiwa viwandani wakiwa na lengo la kuuza mabondo kwenye viwanda vya kuchakata mabondo hayo na kuharibu mazalia ya samaki.

Ameongeza kuwa lazima kuwepo utaratibu maalum kujua upatikanaji wa mabondo hadi kufika kwenye viwanda kwa ajili uchakataji ili samaki wanaovuliwa wawe ni wale ambao wana viwango vinavyotakiwa viwandani kwa ajili ya kuchakatwa.

Kuhusu uvuvi wa dagaa kwa kutumia taa za solar na zana zingine za uvuvi ambapo inaelezwa wavuvi wamekuwa wakivua hadi dagaa ambao wanatakiwa kuwa chakula cha samaki aina ya sangara, Prof. Sheikh amesema serikali itaendelea kufanya taifiti zaidi kwa kuishirikisha Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) ili kuwa na matokeo sahihi.

Amesema kuwa serikali kupitia TAFIRI ni lazima ifanye tafiti za kujiridhisha matokeo yaliyotolewa awali kama yana athari yoyote kabla ya kuwa na matokeo mengine na kuyatolea ufafanuzi ili kuwa na matokeo yasiyokuwa na utata.

Prof. Sheikh amewataka pia wafanyabiashara kuzidi kushirikiana na serikali katika juhudi za kukuza Sekta ya Uvuvi kwa kuunga mkono maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kurasimisha sekta hiyo ili iwe endelevu.

Nao baadhi ya wamiliki wa viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi jijini Mwanza, wameiomba serikali kupitia Wizara ya Uvuvi kuzidi kuchukua hatua katika kupambana na uvuvi haramu ili samaki wazidi kuzaliana kwa wingi na kuongeza wingi wa samaki katika viwanda.

Aidha, wamesema ni muhimu kulinda soko la nje katika kuuza mazao ya uvuvi ili kuliongezea taifa mapato zaidi na kuchangia kwa kiasi kikubwa katika pato la taifa.

Katika kikao hicho ambacho Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekuwa ikiwazungukia wadau mbalimbali wa Sekta ya Uvuvi kupata maoni yao ya namna ya kulinda rasilimali za uvuvi, imesema itakuwa inafanya vikao mara kwa mara ili kutatua changamoto zinazowakabili.

Kabla ya kikao hicho Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh alifika katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza na kufanya mazungumzo na Katibu Tawala wa mkoa huo Bw. Balandya Elikana kuhusu hali ya Sekta ya Uvuvi Mkoani Mwanza ambapo aliarifiwa kuwa uongozi wa mkoa umekuwa ukihakikisha unalinda rasilimali za uvuvi ili ziwanufaishe wananchi wa mkoa huo na taifa kwa ujumla.


Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh akizungumza leo (05.03.2024) jijini Mwanza na wamiliki wa viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi katika jiji hilo, wakati akimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe, ambapo amesema serikali itahakikisha inaweka utaratibu ili kujiridhisha namna ya upatikanaji wa mabondo ya samaki. (05.03.2024)

Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Bw. Balandya Elikana (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh (wa pili kutoka kushoto) na watendaji wengine kutoka wizarani na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, mara baada ya Prof. Sheikh kufika katika ofisi hizo na kuzungumza na katibu tawala huyo namna ya kulinda rasilimali za uvuvi kabla ya kufanya kikao na wamiliki wa viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi jijini Mwanza, akimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe. (05.03.2024)

Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh (mwenye koti jeusi, mstari wa mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya watendaji kutoka wizarani na wamiliki wa viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi jijini Mwanza, baada ya kuahirisha kikao ambapo Prof. Sheikh alipata fursa ya kusikiliza maoni na changamoto zinazowakabili wamiliki hao, akimwakilisha Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo Uvuvi Prof. Riziki Shemdoe. (05.03.2024)




TANZANIA YAKABIDHIWA BOTI KUDHIBITI UVUVI HARAMU

Na. Edward Kondela

Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekabidhiwa boti mbili kutoka Taasisi ya Uvuvi ya Ziwa Victoria (LVFO) ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa ajili ya kufanya doria na kudhibiti uvuvi haramu ndani ya Ziwa Victoria.

Akikabidhiwa boti hizo pamoja na injini tatu na redio maalum kwa ajili ya mawasiliano leo (04.03.2024) jijini Mwanza, Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh amesema vifaa hivyo vitasaidia katika juhudi za serikali kulinda, kuendeleza na kukuza rasilimali za uvuvi ndani ya Ziwa Victoria na Tanzania kwa ujumla.

Amesema anamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya kukuza Sekta ya Uvuvi na kukuza mahusiano katika nchi tatu za Tanzania, Kenya na Uganda ambazo zinatumia Ziwa Victoria.

Ameongeza kuwa lengo la serikali ni kuhakikisha inalinda rasilimali za uvuvi huku akitaja hatua ambazo zimechukuliwa ikiwemo ya Rais Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan Januari 30 mwaka huu, ambapo aligawa boti za uvuvi za kisasa 55 kati ya 160, lengo likiwa ni kuwawezesha wavuvi kuwa na vifaa bora kwa ajili ya uvuvi ndani ya Ziwa Victoria.

Amebainisha kuwa LVFO wameamua kuja na mradi wa pamoja ili kulinda rasilimali za uvuvi wakiwezeshwa na Umoja wa Ulaya ili kuhakikisha samaki wanapatikana kwa wingi na kufikishwa viwandani kwa ajili ya kuchakatwa.

Pia, amesema baada ya kukabidhiwa vifaa kutakuwa na mafunzo kwa maofisa ili kuhakikisha wanapambana na uhalifu wa uvuvi haramu kwa kutumia njia za kisasa na kuwakamata wahalifu.

Kwa upande wake Bw. Lukunya Edward akimwakilisha Katibu Mtendaji wa LVFO wakati wa kukabidhi boti hizo kwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, amesema vifaa hivyo vitatumika zaidi katika kudhibiti uvuvi haramu na kutunza rasilimali za uvuvi.

Amefafanua kuwa katika kudhibiti uvuvi haramu kutasaidia kukuza samaki kwa wingi na kuongeza upatikanaji wa samaki na kuwezesha jamii zilizopo katika ukanda wa Ziwa Victoria kunufaika na mazao ya uvuvi.

Tanzania kukabidhiwa boti mbili zenye thamani ya takriban Shilingi Milioni 100 pamoja na vifaa vingine kwa ajili ya doria ndani ya Ziwa Victoria ni mradi uliopita kwenye Taasisi ya Uvuvi ya Ziwa Victoria (LVFO) ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambapo jumla ya boti sita na injini tisa zimegaiwa kwa nchi tatu za Tanzania, Kenya na Uganda.


Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh (wa kwanza kulia) akikagua boti mbili za doria kwa ajili ya kudhibiti uvuvi haramu ndani ya Ziwa Victoria, kabla ya kukabidhiwa boti hizo kwa serikali kutoka Taasisi ya Uvuvi ya Ziwa Victoria (LVFO) ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. (04.03.2024)

Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh (mwenye koti jeusi, katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya watendaji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Taasisi ya Uvuvi ya Ziwa Victoria (LVFO) ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, wakati wa hafla fupi ya kukabidhiwa boti mbili za doria kwa serikali ili kudhibiti uvuvi haramu ndani ya Ziwa Victoria. (04.03.2024)

Moja ya boti za kudhibiti uvuvi haramu ndani ya Ziwa Victoria, iliyokabidhiwa kwa serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi ikiwa kwenye majaribio, ambapo Tanzania imekabidhiwa boti mbili zenye thamani ya takriban Shilingi Milioni 100 pamoja na vifaa vingine kwa ajili ya doria ndani ya Ziwa Victoria kupitia mradi wa Taasisi ya Uvuvi ya Ziwa Victoria (LVFO) ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambapo jumla ya boti sita na injini tisa zimegaiwa kwa nchi tatu za Tanzania, Kenya na Uganda. (04.03.2024)


 








WAFUGAJI MSOMERA WAZURU LITA, TALIRI TANGA

Wafugaji kutoka kijiji cha Msomera kilichopo Handeni mkoani Tanga leo februari 28, 2024 wametembea taasisi za Wakala ya Mafunzo ya Mifugo nchini (LITA) kampasi ya Buhuri mkoani humo na ile ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kanda ya Mashariki ambapo wamefurahishwa na elimu ya ufugaji waliyoipata kwenye Taasisi hizo.

Akizungumza mara baada ya kukamilisha ziara hiyo ya siku moja, Mwenyekiti wa Kijiji cha Msomera Bw. Martin Paraketi ambaye mbali na kuishukuru Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Taasisi zake kwa kuwawezesha fursa hiyo ya mafunzo amewataka wafugaji wa kijiji chake kuwa mabalozi kwa wafugaji wengine kupitia yale waliyojifunza kutoka kwa wataalam wa taasisi zake.

"Tunatambua Serikali imetambua umuhimu wetu kuja kujifunza hapa ili tushirikiane na wataalam wake kutoa elimu ya ufugaji bora kwa wenzetu tuliowaacha huko hivyo nitoe rai kwa wenzangu kila mmoja kutimiza wajibu wa kuelimisha kaya inayomzunguka kule Msomera" Amesema Bw. Paraketi

Aidha Bw. Paraketi ameiomba Serikali kuwashirikisha wananchi wa kijiji chake wakati wote wa utafiti wa masuala mbalimbali yanayolenga ufugaji bora jambo ambalo anaamini litazidi kuongeza ujuzi kwa wafugaji waliopo kijijini hapo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa TALIRI kanda ya Mashariki Dkt. Zabron Nziku amewahamasisha wafugaji hao kuchangamkia fursa ya biashara ya malisho ya Mifugo inayoonekana kuongezeka thamani kadri siku zinavyoenda.

"Kwa sasa mbegu za malisho aina ya "cenchrus" zinauzwa shilingi 25,000 kwa kilo na hiyo ni kwa bei ya Serikali lakini kwa upande wa Taasisi binafsi zinauzwa 35,000 hadi 40,000 kwa kilo hivyo niwaombe mgeukie na kwenye fursa hii itakayowasaidia sana" Amesema Bw. Nziku.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha ziara hiyo, Mkugenzi wa Utafiti, Mafunzo na Ugani kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Angelo Mwilawa amesema kuwa ziara hiyo ni miongoni mwa jitihada za Serikali kupitia Wizara yake katika kuhakikisha wafugaji wa kijiji cha Msomera wanajifunza kwa vitendo namna ya kufanya ufugaji bora na wenye tija.

"Taasisi hizi ni zenu na mnakaribishwa kuzitembela na kujifunza wakati wowote hata kama mtawezeshwa na wadau wengine kufanya hivyo na sisi tunaangalia namna ya kuja kutoa mafunzo kwenye vitongoji vya Olmolot, Urkung'u, Mkababu, katikati na eneo lote la "area F" Ameongeza Dkt. Mwilawa.

Mbali na kupewa elimu ya uzalishaji na utunzaji wa malisho bora ya mifugo, wafugaji hao wa kijiji cha Msomera walipewa mbegu za malisho hayo ili wakapande kwenye eneo watakalotumia kama shamba darasa kijijini kwao.


Mkurugenzi wa Utafiti, Mafunzo na Ugani kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Angelo Mwilawa (kushoto) akiwaelimisha wafugaji wa kijiji cha Msomera kuhusu kilimo cha Malisho bora ya Mifugo walipofika kwenye Shamba la Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kanda ya Mashariki mkoani Tanga Februari 28, 2024.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) kanda ya Mashariki Dkt. Zabron Nziku (kushoto) akiwaeleza wafugaji wa kijiji cha Msomera kuhusu shughuli zinazofanywa na TALIRI kwenye kanda hiyo muda mfupi walipowasili hapo februari 28, 2024 mkoani Tanga.

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo nchini (TALIRI) Prof. Erick Komba (kushoto) akimkabidhi Mwenyekiti wa kijiji cha Msomera Bw.Martin Paraketi sehemu ya mbegu za malisho ya Mifugo zitakazopandwa kwenye shamba darasa la kijiji hicho wakati wa ziara ya wafugaji hao kwenye Taasisi hiyo kanda ya Mashariki mkoani Tanga februari 28, 2024.




  

WIZARA YAZIDI KUKUTANA NA WADAU WA UVUVI KUTEKELEZA AGIZO LA MHE. RAIS DKT. SAMIA SULUHU HASSAN

Na. Edward Kondela

Wizara ya Mifugo na Uvuvi inaendelea kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan la kuwataka watendaji wa wizara hiyo kuendelea kuwatembelea wadau wa Sekta ya Uvuvi ili kutatua changamoto zao.

Naibu Katibu Mkuu (Uvuvi) Bi. Agness Meena amebainisha hayo leo (28.02.2024) katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam wakati wa kikao cha wadau wa viwanda na biashara ya mazao ya uvuvi ili kusikiliza hoja zao na changamoto zinazowakabili.

Bi. Meena amesema wizara inataka kupunguza changamoto zilizopo katika Sekta ya Uvuvi kwa kufanya mikutano na wadau na kufanya maboresho yakiwemo ya kisera na kisheria ili sekta hiyo izidi kutoa mchango mkubwa zaidi katika pato la taifa.

Amebainisha kuwa kupitia hotuba aliyotoa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa kugawa boti na vizimba jijini Mwanza, amesema lengo la serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi ni kutatua changamoto za sekta hiyo kupitia vikao endelevu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh amesema wizara imepokea maoni yote yaliyotolewa na wadau hao na kwamba watahakikisha yanafanyiwa kazi na kwamba katika kikao kijacho hoja zao zitakuwa zimefanyiwa kazi.

Amesema katika kikao hicho wadau hao hawapaswi kukata tamaa kwa kuwa baadhi ya hoja huenda zikawa zinafanyiwa kazi hatua kwa hatua hadi kufikia muafaka.

Nao baadhi ya wadau wa viwanda na biashara ya mazao ya uvuvi waliohudhuria kikao hicho wamepongeza namna serikali inavyoendelea kuwajali na kuwapa fursa ya kuwasikiliza huku wakishauri hatua zaidi ziendelee kuchukuliwa ikiwemo elimu dhidi ya uvuvi haramu.

Wameongeza kuwa kwa sasa serikali imechukua hatua kubwa katika kulinda rasilimali za uvuvi huku wakiomba kuboreshwa zaidi kwa mazingira ya uwekezaji ili wapate masoko zaidi ya mazao hayo hususan nje ya nchi.

Wizara ya Mifugo na Uvuvi inaendelea na vikao vya kukutana na wadau wa Sekta ya Uvuvi maeneo mbalimbali nchini ili kupata maoni na hoja za wadau hao ili zifanyiwe kazi lengo likiwa ni kukuza zaidi na kuongeza tija katika sekta hiyo.


Naibu Katibu Mkuu (Uvuvi) Bi. Agness Meena akizungumza wakati wa kikao cha wadau wa viwanda na biashara ya mazao ya uvuvi kilichofanyika katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam, ambapo amesema Wizara ya Mifugo na Uvuvi inaendelea kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan la kuwataka watendaji wa wizara hiyo kuendelea kuwatembelea wadau wa Sekta ya Uvuvi ili kutatua changamoto zao. (28.02.2024)

Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh akizungumza wakati wa kikao cha wadau wa viwanda na biashara ya mazao ya uvuvi kilichofanyika katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam, ambapo amewahakikishia wadau hao kuwa maoni yao yatafanyiwa kazi na kupatiwa mrejesho katika vikao vijavyo ili kukuza Sekta ya Uvuvi nchini. (28.02.2024)


Picha ya pamoja ya Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Bi. Agness Meena (wa tano kutoka kulia, mstari wa kwanza) akiwa na baadhi ya watendaji kutoka wizarani na wadau wa viwanda na biashara ya mazao ya uvuvi, baada ya kikao kilichofanyika katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam ili kusikiliza maswali na hoja zao katika kukuza Sekta ya Uvuvi nchini. (28.02.2024)



VIBALI VYA UVUVI KWA NJIA YA KIELETRONIKI NDANI YA SIKU SABA

Na. Edward Kondela

Serikali imesema katika kipindi kifupi kijacho itahakikisha vibali vinavyohusu masuala ya uvuvi vinatolewa kwa njia ya kieletroniki ndani ya siku saba.

Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh amesema hayo leo (27.02.2024) katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam, wakati alipofanya kikao kifupi na baadhi ya wadau wa uvuvi wanaojishughulisha na uuzaji wa nyavu za uvuvi.

Prof. Sheikh amesema kuwa mfumo wa kutoa vibali kwa njia ya kieletroniki utawezesha kutolewa vibali ndani ya siku saba ili kurahisisha huduma kwa wadau wa Sekta ya Uvuvi kupata vibali popote walipo.

Ameongeza kuwa mikakati ya wizara ni kwamba kabla ya kuisha kwa mwaka wa fedha 2023/24 inatarajia kuanza rasmi utoaji wa vibali hivyo kwa nji ya kieletroniki.

Ameongeza kuwa nia ya serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kupunguza ucheleweshaji wa vibali na kuifanya Sekta ya Uvuvi kuchangia kwa kiasi kikubwa katika pato la taifa.

Katika kikao hicho pia Prof. Sheikh amepata muda wa kuwaarifu wadau hao mikakati mbalimbali ya serikali katika kukuza Sekta ya Uvuvi pamoja na kujibu hoja na maswali mbalimbali kutoka kwa wadau juu ya kuimarisha sekta hiyo.

Baadhi ya wadau wa Sekta ya Uvuvi wanaojishughulisha na uuzaji wa nyavu za uvuvi waliohudhuria kikao hicho, wamepongeza namna serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi inavyofanya jitiohada mbalimbali za kukuza sekta hiyo ikiwemo ya kuhakikisha uwepo wa zana bora za uvuvi.

Wamesema wako pamoja na serikali katika kuhakikisha uvuvi haramu unadhibitiwa ili kulinda rasilimali za uvuvi na kuomba uwepo wa mikakati zaidi ya kudhibitiwa kwa nyavu haramu ambao hazitakiwi nchini. 


Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh akizungumza na baadhi ya wadau wa Sekta ya Uvuvi (hawapo pichani) wanaojishughulisha na uuzaji wa nyavu za uvuvi ambapo amewahakikishia kuwa katika kipindi kifupi kijacho serikali itaanza kutoa vibali vinavyohusu masuala ya uvuvi kwa njia ya kieletroniki ndani ya siku saba. Kikao hicho kimefanyika katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam. (27.02.2024)

Mratibu wa mradi wa Uendelezaji wa Rasilimali za Uvuvi na Ukuzaji Viumbe Maji (TASFAM) kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Nichrous Mlalila akisikiliza hoja mbalimbali kutoka kwa wadau wa Sekta ya Uvuvi wanaojishughulisha na uuzaji wa nyavu za uvuvi, wakati wa kikao alichohitisha Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh (hayupo pichani) na wadau hao kilichofanyika katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam. (27.02.2024)

Picha ya pamoja ya Mkurugenzi wa Idara ya Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh (wa tatu kutoka kulia, mstari wa mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wadau wa Sekta ya Uvuvi wanaojishughulisha na uuzaji wa nyavu za uvuvi na maafisa kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, baada ya kikao kilichofanyika katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam, kujadili namna ya kuboresha sekta hiyo. (27.02.2024)


WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI KUTATUA CHANGAMOTO ZA WAVUVI

 



Mkuu wa Wilaya ya Sengerema Mhe. Senyi Ngaga akifungua kikao cha kujadili changamoto mbalimbali zinazowakabili wanufaika wa boti na vizimba na hivyo kuzipati utatuzi, Aidha amewasihi wanufaika kutumia vifaa hivyo kama ilivyokusudiwa na kurejesha mikopo yao kwa uaminifu,  Februari 24,2024 Mkoani Mwanza.

 

Mkurugenzi wa Ukuzaji Viumbe maji Dkt. Nazaeli Madalla akifafanua baadhi ya hoja zilizoibuliwa  na wanufaika wa mkopo wa vizimba usio na riba  wakati wa kikao kifupi cha kusikiliza changamoto mbalimbali za wanufaika hao kilichofanyika  Buchosa Mkoani Mwanza, Februari 24,2024

Kaimu Mkurugenzi  Msaidizi Ukuzaji Viumbe Maji Baridi, Dkt. Imani Kapinga akujibu baadhi ya maswali yaliyokuwa yakiulizwa  na baadhi ya wanufaika wa mkopo wa  vizimba usio na riba  (hawapo pichani)  wakati wa kikao kifupi cha kusikiliza na kujibu changamoto  zinazowakabili wanufaika hao kilichofanyika Buchosa  Mkoani Mwanza, Februari 24,2023

Mkurugenzi msaidizi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani, (uvuvi) Bw. Anthony Dadu (aliyesimama) akijibu maswali mbalimbali yaliyojitokeza wakati wa kikao kifupi cha kujadili changamoto mbalimbali zinazowakabili wanufaika wa mkopo wa  vizimba na maboti, Februari 24,2024 Mkoani Mwanza

Afisa Maendeleo ya Biashara kutoka Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) Bi. Glacia Marugujo (katikati) akitoa maelezo kwa wanufaika wa mkopo nafuu usio na riba  wa boti na vizima juu ya namna na siku watakayoanza kurejesha  mikopo hiyo Februari 24,2024 Mkoani Mwanza.

Katibu wa kikundi cha Sangara - Nyakaliro Ficos Bw. Revocatus Rugaba akieleza changamoto mbalimbali na kutoa maoni kwa Mkuu wa Wilaya ya Sengerema Mhe. Senyi Ngaga na watendaji kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) (hawapo pichani) wakati wa kikao kifupi cha kujadili changamoto hizo na kuzipatia utatuzi, kikao hicho kimefanyika Buchosa Mkoani Mwanza Februari 24, 2024











Jumatano, 6 Machi 2024

SERIKALI YAZINDUA BBT-LIFE (UVUVI) AWAMU YA PILI.

 Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na wenye ulemavu imezindua awamu ya pili ya program ya Jenga kesho iliyo bora kwa wanawake na vijana kwa upande wa sekta ya Uvuvi maarufu kama “BBT-LIFE” tukio lililofanyika leo februari 23, 2024 kwenye  Wakala ya Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kampasi ya Mbegani Bagamoyo mkoani Pwani.

Uzinduzi huo ambao umetanguliwa na mafunzo ya siku 5 ya kubadili fikra kwa vijana na wanawake 300 waliochaguliwa kunufaika na awamu ya pili  program hiyo umefanywa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Bi. Agness Meena ambaye amewasisitiza vijana hao kuhakikisha wanatumia vema mafunzo kwa vitendo watakayopewa kwa muda wa miezi 3 kwenye vituo walivypangiwa baada ya kukamilika kwa mafunzo hayo ya Nadharia.

“Baada ya kukamilika kwa mafunzo ya siku 5 ya “mind-set transformation” mnaenda kwenye mafunzo kwa vitendo kwa muda wa miezi 3, nitoe rai kwenu wote mkazingatie yale yote mtakayojifunza huko ili mkitoka huko muweze kujiajiri na kuajiri wenzenu ambao hawakupata fursa ya kushiriki kwenye programu kwa awamu hii” Amesema Bi. Meena.

Bi. Meena ameongeza kuwa lengo la Wizara yake ni kutengeneza vijana na wanawake watakaokuwa wajasiriamali wakubwa kwenye upande wa sekta ya Uvuvi kupitia ufugaji wa samaki kwenye  vyanzo vya asili vya maji chumvi na baridi, mabwawa na kilimo cha zao la mwani.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na wenye ulemavu Bw.Robert Masingiri amebainisha kuwa utekelezaji wa awamu ya pili ya programu ya BBT-LIFE ni sehemu ya utekelezaji wa program ya Taifa ya kukuza ujuzi nchini kupitia kipengele cha mafunzo ya wanagenzi.

“Programu hii yote inagharamiwa na Serikali na kila mwaka huwa inatenga kiasi cha Bil.9 kwa ajili ya kuhakikisha vijana na wanawake wanapata ujuzi stahiki ili waweze kujiajiri na mpaka sasa imeshatoa kiasi cha shilingi Bil. 5.5 kwa ajili ya utekelezaji wa program hiyo” Amesizitiza Bw. Masingiri.

Akizungumzia namna Taasisi yake ilivyojipanga kuwawezesha mikopo wahitimu wa program hiyo, Mwakilishi wa benki ya Maendeleo ya Kilimo nchini (TADB) Bw. Kezilahabi Jumanne amesema kuwa walipata nafasi ya kutoa elimu ya uandaaji maandiko ya kibiashara kwa wanufaika hao hivyo anaamini baada ya kuhitimu mafunzo hayo baadhi yao watakuwa wateja wao wa moja kwa moja kupitia mikopo watakayowawezesha.

Wakizungumza kwa niaba ya wanufaika wenzao wao, Mshiriki kutoka Zanzibar Bi. Samia Othman na mwingine kutoka Kagera Bw. Marius Juvinali wameishukuru Serikali kwa kuwawezesha kuingia kwenye awamu ya pili ya programu ya BBT-LIFE ambapo wameahidi kuzingatia yale yote watakayoelekezwa wakati wa mafunzo kwa vitendo kwenye vituo walivyopangiwa.

Utekelezaji wa programu ya “Jenga Kesho iliyo bora kwa wanawake na vijana kupitia sekta ya Uvuvi kwa mwaka huu unafanyika kwa mara ya pili ambapo kwa mwaka jana Programu hii ilihusisha vijana na wanawake 200 kutoka maeneo mbalimbali ya Tanzania.


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agness Meena (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na wanufaika wa BBT-LIFE waliokuwa na changamoto ya usikivu hafifu Bw. Sayid Ngasa (kulia nyuma) na Bi. Maria Mahona (katikati nyuma) muda mfupi baada ya uzinduzi wa programu hiyo uliofanyika Leo Februari 23, 2024 Bagamoyo mkoani Pwani. Kushoto nyuma ni Mtafsiri wao wa lugha ya alama Bw. Mmanga Haji.  Wengine pichani ni Mkurugenzi Msaidizi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na wenye ulemavu Bw. Robert Masingiri (kulia mbele) na Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Uvuvi (FETA) Dkt. Semvua Mzighani.


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Agness Meena (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na wanufaika wa awamu ya pili ya programu ya BBT-LIFE (Uvuvi) muda mfupi baada ya uzinduzi wa programu hiyo uliofanyika Leo Februari 23, 2024 Bagamoyo mkoani Pwani. Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na wenye ulemavu Bw. Robert Masingiri na kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Vyuo vya Mafunzo ya Uvuvi (FETA) Dkt. Semvua Mzighani.

 

BBT-LIFE (UVUVI) AWAMU YA PILI YANG'OA NANGA


Wanufaika waanza kupigwa msasa

Serikali kupitia wizara ya Mifugo na uvuvi imeanza kutekeleza programu ya "Jenga kesho iliyo bora kwa wajasiriamali wanawake na vijana upande wa sekta ya Uvuvi kupitia mafunzo yanayotolewa kwa vijana na wanawake 300 kutoka pande  mbalimbali za nchi yaliyoanza kutolewa februari 19, 2024 kwenye chuo cha mafunzo ya uvuvi (FETA) kampasi ya Mbegani Bagamoyo mkoani Pwani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa wizara hiyo Bi. Imelda Adam amewataka washiriki wa programu hiyo kuzingatia yale yote watayoelekezwa wakati wote wa mafunzo hayo ya nadharia yatakayofanyika kwa siku 5 ili waweze kufanya vizuri watakapoenda vituoni kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo.

"Programu hii inalenga kuwageuza wahitimu wa ngazi mbalimbali kwenye kada ya Uvuvi kuweza kujiajiri badala ya kusubiri kuajiriwa na lengo la Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha vijana na wanawake wengi zaidi wanawezeshwa kupitia programu hii" Amesema Bi Imelda.

Aidha Bi. Imelda amewataka washiriki hao kutobweteka na kiasi cha fedha wanachopewa na Serikali kwa ajili ya kujikimu wakati wote wa mafunzo na badala yake wajikite kwenye mtazamo wa kuandaa kesho yao iliyo bora baada ya kuhitimu mafunzo hayo.

Kwa upande wake Afisa Uvuvi Mwandamizi kutoka Wizarani hapo Bw. Clemence Katunzi amewataka wanufaika hao kuhakikisha elimu watakayoipata mara baada ya kuhitimu mafunzo huo wanaipeleka kwenye jamii zinazowazunguka katika maeneo yao.

"Tutawapanga kwenye vituo mbalimbali ambavyo vitakuwa jumuishi na awamu hii tutakuwa na vituo 17 ambapo kimoja upande wa Zanzibar na 16 vipo Tanzania bara" Ameongeza Bw. Katunzi.

Utekelezaji wa programu ya Jenga kesho iliyo bora kwa wajasiriamali wanawake na vijana awamu ya pili unatarajiwa kuchukua miezi 3 mara baada ya kukamilika kwa mafunzo kwa nadharia yanayofanyika kuanzia Februari 19-23, 2024.


Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi. Imelda Adam (kulia) akizungumza na wanufaika wa programu ya BBT-LIFE (Uvuvi) awamu ya pili wakati wa ufunguzi wa programu hiyo uliofanyika leo Februari 19, 2024 kwenye Chuo cha Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kampasi ya Mbegani wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani.

 

Afisa Uvuvi Mwandamizi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Clemence Katunzi (kulia) akifafanua namna programu ya BBT-LIFE (Uvuvi) awamu ya pili itakavyotekelezwa  wakati wa ufunguzi wa programu hiyo uliofanyika leo Februari 19, 2024 kwenye Chuo cha Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kampasi ya Mbegani wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani.


 

MHE. ULEGA ARIPOTI SENTRO

 


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (kulia) akifafanua jambo wakati akizungumza na Watangazaji wa Kipindi cha Sentro kinachorushwa na Clouds TV moja kwa moja  kutoka jijini Dodoma Februari 9, 2024.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (wa pili kulia) akizungumza na Watangazaji wa Kipindi cha Sentro kinachorushwa na Clouds TV moja kwa moja kutoka jijini Dodoma  Februari 9, 2024.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watendaji wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Watangazaji wa Kipindi cha Sentro kinachorushwa na Clouds TV muda mfupi baada ya kumaliza kushiriki katika kipindi hicho kutokea jijini Dodoma leo Februari 9, 2024.

 


DKT. MPANGO: “WEKENI JICHO LA PEKEE LONGIDO, WANAHITAJI MAJI NA MALISHO.”

Na. Edward Kondela

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ameitaka Wizara ya Mifugo na Uvuvi kutoa jicho la pekee katika Wilaya ya Longido Mkoani Arusha kwa kuongeza mabwawa ya kunyweshea mifugo na kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii kulinda malisho.

Makamu wa Rais Mhe. Dkt. Mpango amebainisha hayo leo (10.02.2024) Wilayani Longido akiwa kwenye ziara ya kikazi wakati akizindua Kituo cha Afya Ketumbeine na mradi wa kusambaza umeme vijijini awamu ya tatu mzunguko wa kwanza unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

Ameongeza kuwa mabwawa yanayoonesha udhaifu yakarabatiwe na hiyo ndiyo itakuwa zawadi kwa wakazi wa Wilaya ya Longido kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Ndugu zangu hawa ni wafugaji, mmeanza kazi vizuri lakini, ninawataka tena kutoa jicho la pekee kwa Wilaya ya Longido, kuongeza mabwawa ya kunyweshea mifugo yao na kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii kulinda malisho na mabwawa yanayoonesha udhaifu yakarabatiwe.” Amesema Mhe. Dkt. Mpango

Mhe. Dkt. Mpango amebainisha hayo baada ya Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Arusha Bw. Thomas Ole Sabaya kumueleza Makamu wa Rais kuwa wafugaji hawana kazi nyingine zaidi ya kufuga hivyo wanategemea sana maeneo yao kwa ajili ya kufuga na malisho.

Pia, ameiomba serikali iwasaidie kuweka utaratibu ukiwemo wa wawekezaji wanaotaka kuwekeza kwenye maeneo yao ili kulinda maeneo ya malisho wakati wote hali itakayoondoa ufugaji wa kuhamahama na kusababisha migogoro maeneo mengine.

Naye Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti amesema wizara imeendelea kusogeza huduma mbalimbali kwa wafugaji wa Wilaya ya Longido ikiwa ni pamoja na kuchimba mabwawa makubwa kwa ajili ya kusambaza maji kwa mifugo pamoja na majosho.

Mhe. Mnyeti amefafanua kuwa katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2023/24 serikali imetenga Shilingi Milioni 46 kwa ajili ya kujenga majosho mawili katika vijiji vya jirani pamoja na josho kubwa ambalo tayari limezinduliwa mwaka jana.

Aidha, amesema kutokana na ukame katika baadhi ya maeneo serikali itahakikisha inaendelea kusogeza maji karibu kwa kushirikiana na Wizara ya Maji ili wafugaji waweze kupata maji kwa ajili ya matumizi ya binadamu na mifugo.

Pia, amesema wizara kwa sasa inaendelea kuhamasisha ujengaji wa mabwawa ya kufugia samaki na kuiasa jamii ya kimasai kula samaki kama ambavyo baadhi yao wameanza kula.

Makamu wa Rais Mhe. Dkt. Philip Mpango akiwa kwenye ziara ya kikazi katika Wilaya ya Longido Mkoani Arusha, ambapo aliambatana na mkewe Mama Mbonimpaye Mpango amezindua pia mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari ya wasichana Longido Samia, utakaogharimu Shilingi Bilioni Tatu.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akizungumza wakati wa uzinduzi wa Kituo cha Afya Ketumbeine na mradi wa kusambaza umeme vijijini awamu ya tatu mzunguko wa kwanza unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) katika Wilaya ya Longido Mkoani Arusha, ambapo ameitaka Wizara ya Mifugo na Uvuvi kutoa jicho la pekee katika wilaya hiyo kwa kuongeza mabwawa ya kunyweshea mifugo na kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii kulinda malisho. (10.02.2024)

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti akizungumza katika ziara ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango katika Wilaya ya Longido Mkoani Arusha, ambapo amesema wizara imeendelea kusogeza huduma mbalimbali kwa wafugaji wa Wilaya ya Longido ikiwa ni pamoja na kuchimba mabwawa makubwa kwa ajili ya kusambaza maji kwa mifugo pamoja na majosho. (10.02.2024)

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akisalimiana na viongozi mbalimbali akiwemo Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti (kulia) wakati alipofanya ziara ya kikazi katika Wilaya ya Longido Mkoani Arusha. (10.02.2024)

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akiwa kwenye moja ya picha za pamoja na viongozi mbalimbali akiwemo Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Alexander Mnyeti, wakati alipofanya ziara ya kikazi katika Wilaya ya Longido Mkoani Arusha. (10.02.2024)


PROF. SHEMDOE AKUTANA NA MWAKILISHI MKAAZI WA SHIRIKA LA JICA

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe amekutana na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Maendeleo la Japan (JICA), Bw. Ara Hitoshi kujadiliana utekelezaji wa makubaliano ya kuendeleza mradi wa Afya Moja unaoangalia magonjwa yanayoambukizwa kutoka kwenye Mifugo kwenda kwa binadamu  ikiwepo Brucellosis na Kifua Kikuu (TB).

Prof. Shemdoe amekutana na Mwakilishi huyo Ofisini kwake Mtumba, jijini Dodoma Januari 7, 2024.

Mradi huo unasimamiwa na Wataalamu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Maprofesa kutoka Chuo cha Kilimo cha Sokoine (SUA) na Maprofesa kutoka Chuo cha Mifugo cha Rakuna, kilichopo katika Mji wa Hokaido nchini Japan.

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe akizungumza na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Maendeleo la Japan (JICA), Bw. Ara Hitoshi (kulia) alipokutana nae Ofisini kwake Mtumba, jijini Dodoma Januari 7, 2024.

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Maendeleo la Japan (JICA), Bw. Ara Hitoshi (kushoto) baada kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika Ofisini kwake Mtumba, jijini Dodoma Januari 7, 2024.

Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Riziki Shemdoe (katikati)akiagana na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Maendeleo la Japan (JICA), Bw. Ara Hitoshi (kushoto) muda mfupi baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika Ofisini kwake Mtumba, jijini Dodoma Januari 7, 2024.